Correspondance Course - Lesson 09

Swahili

Somo la 9

UFALME WAKO UJE

SOMO : 1 Nyakati 29

“Ufalme wako uje. Mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama mbinguni”.

Ni mara ngapi umeyasema maneneo haya, au kuyasikia yakitamkwa na wengine? Yapo yakiwa ni sehemu ya maombi, ambayo Yesu aliwafundisha wanafunzi wake. Unaweza kuyasoma katika Luka 11:2-4. Tunayafahamu maneno haya vizuri, lakini unajua yanachokimaanisha?

Yaangalie tena. Ni maombi kwamba Ufalme wa Mungu uweze kuja ili mapenzi yake Mungu yaweze kutendeka katika dunia hii, kama yanavyofanywa wakati wote huko mbinguni. Kwa hiyo tunaona moja kwa moja kuwa, Ufalme ambao tunauombea ni wa kuwa hapa duniani, na kwamba, Ufalme huo wa Mungu ukija, ndipo watu watakapoyatimiza anayoyapenda Mungu, katika dunia hii.

Nchi kwa ajili ya Ufalme

 Ufalme ni lazima uwe na mahali, na miaka elfu kadhaa iliyopita Mungu aliichagua nchi ambayo itakuwa  Makao-Makuu ya Ufalme wake; ni nchi ya Israeli.

Yerusalemu ni Mji-Mkuu wa Israeli, na ndio utakaokuwa ‘kitovu’ cha utawala wa dunia, wakati Yesu Kristo akiwa Mfalme. Yesu mwenyewe alisema:

“Usiape kabisa,  hata  kwa mbingu, kwa  maana ndicho kitu cha enzi cha Mungu; wala kwa  nchi, kwa  maana ndiyo pa kuwekea miguu yake; wala Yerusalemu, kwa maana ndio mji wa Mfalme mkuu” (Mathayo 5:34,35).

Yesu aliyapata maneno haya kwenye Zaburi ya 48; kitu kinachotudokezea kwamba, tunapaswa kulisoma Agano la Kale nalo vizuri. Msitari wa pili wa Zaburi hiyo unasema hivi juu ya mlima Sayuni, mahali Yerusalemu ilipo:

 â€œKuinuka kwake ni mzuri sana, ni furaha ya dunia yote, mlima Sayuni pande za kaskazini; mji wa Mfalme mkuu” (Zab.48:2).

Mlima Sayuni ni sehemu ya Yerusalemu na hapa unaelezewa kuwa, “Ni furaha ya dunia yote”. Zaburi ya pili nayo inasema: “Nami nimemweka mfalme wangu juu ya Sayuni, mlima wangu mtakatifu”. (Zab.2:6).

Zaburi hii ni unabii unaohusu wakati Yesu atakapokuwa akitawala kutoka katika mlima Sayuni. Mungu alichagua ‘kuliweka Jina lake’ katika jiji la Yerusalemu miaka mingi nyuma.  Katika 2 Nyakati 6:5;6 alishasema: “…Lakini nimeuchagua Yerusalemu, jina langu liwe humo”.

Hapa kuna vifungu vingine viwili kwa ajili yako kuvisoma kiuangalifu:

  1. Isaya 62:1-7: Tunatakiwa kumwomba Mungu aifanye Yerusalemu kuwa mahali pa sifa duniani (‘taji ya uzuri’).
  2. Isaya 65:l7-25:  Mungu anaweka mpango wake juu ya Yerusalemu, na anatutaka tuufurahie.

Kuliwahi kuwa na Ufalme wa Mungu katika dunia hii miaka mingi iliyopita, katika Agano la Kale.  Je, unalifahamu hilo?. Fungua sasa 1 Nyakati 29, na soma msitari wa kwanza, na wa 10 mpaka wa l3. Msitari wa 11, unasema:

“Ufalme ni wako, Ee BWANA, nawe umetukuzwa, u mkuu juu ya vitu vyote” (1 Nyakati 29:11).

Ufalme unaoongelewa, kama utakavyoona unavyoendelea kukisoma kifungu hiki, ni Ufalme wa Israeli, katika nchi ya Israeli, kwani tunasoma:

“Ndipo Sulemani akaketi katika kiti cha enzi cha BWANA, awe mfalme badala ya Daudi babaye” (1 Nyakati 29:23).

Kiti cha enzi alichokikalia Daudi na ambacho mwanawe Sulemani alikikalia baada yake, kilikuwa ni mamlaka katika Yerusalemu, mji uliokuwa mkuu katika nchi ya Israeli. Ufalme ambao aliutawala akiwa mfalme ulikuwa Ufalme wa Israeli.

Ni kwa nini Ufalme wa Israeli uliitwa Ufalme wa Mungu, na ‘kiti chake cha enzi’ kiliitwa, “Kiti cha Enzi cha BWANA?”  Sababu ni kwamba:

  1. Ni Mungu mwenyewe aliyewapa Waisraeli Ufalme huo.
  2. Ni Mungu mwenyewe aliyeuteua Yerusalemu kuwa Makao Makuu (1 Wafalme 11:13).
  3. Ni Mungu mwenyewe aliyetoa Sheria za kuuongoza Ufalme huo (Zipo katika vitabu vya Mambo ya Walawi, Hesabu na Kumb. La Torati).
  4. Mfalme alikuwa akitawala kwa niaba ya Mungu.

Ufalme wa Mungu ulipinduliwa

Mamia ya miaka yalipita. Wafalme mmoja baada ya mwingine waliitawala Israeli katika Yerusalemu. Baadhi yao walikuwa wafalme wazuri waliowaongoza watu wao kwa kumcha Mungu, na wafalme wengine walikuwa waovu; wasiozizingatia Sheria za Mungu.

Mwisho ulifika wakati ambao Taifa la Israeli liliziacha mno njia za Mungu na mfalme katika Yerusalemu alikuwa mwovu mno. Mwenyezi Mungu aliamua kuuvunjilia mbali Ufalme huo.

Soma Ezekieli 21:25 – 27, na hasa msitari wa 27 unaosema: “Nitakipindua, nitakipindua, nitakipindua (kiti cha enzi cha Israeli katika Yuda); hiki nacho hakitakuwa tena, hata atakapokuja yeye ambaye ni haki yake, nami nitampa”.

Yeye ambaye ‘ni haki yake’

Tunaweza kuona kutoka katika mistari hiyo ya Ezekiel kuwa, kulikuwa na mtu ‘wa kuja’ ambaye Kiti hicho cha Enzi cha Ufalme wa Mungu kilikuwa ni ‘haki yake’. Huyu alikuwa awe ndiye mrithi wa kukifaa, na Mungu alikuwa amepanga kukimpa.

Tokea wakati huo wa mfalme huyo wa mwisho aliyeng’olewa kutoka katika kiti hicho cha enzi, mpaka sasa, hakujawa na mfalme wa Kiyahudi aliyetawala katika Yerusalemu tena. Lakini fungua Biblia yako kwenye Luka 1:31 – 33 na usome  maneno yaliyosemwa na malaika kwa Mariamu, mama yake Yesu. Akisemea malaika juu ya jina la Yesu, alisema:

Huyo atakuwa Mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye Juu, na Bwana  Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake” (Luka 1:32).

Ni nani aliyekuwa na ‘haki’ ya Kiti cha Enzi cha Ufalme wa Mungu? Hakika ni Yesu, Mwana wa Mungu.  Haki yake ina sura mbili:

  1. Alikuwa ni Mwana wa Mungu.
  2. Mama yake Mariamu alikuwa wa uzao wa Daudi.

Kuna kutokuelewa kwingi kunakohusu utawala wa Yesu katika Ufalme wa Mungu. La muhimu kutambua ni kwamba:

  1. Yesu atakuwa mtawala katika dunia.
  2. Kiti chake cha enzi kitakuwa ni Kiti cha Enzi cha Daudi katika Yerusaremu.
  3. Yerusalemu itakuwa Makao Makuu ya Ufalme wa Mungu duniani.

Hii ndio sababu ya Yesu kurudi duniani. Kusudi la Mungu linawahusu wanadamu katika dunia na atalitimiza, ndio maana Mwenyewe anasema: “Dunia hii nzima itajawa na utukufu wa BWANA”  (Hesabu 14:21).

Kufikiri kwamba mtu anakwenda mbinguni anapokufa, hakwendani na Maandiko; hakukubaliani na kile Maandiko yanachofundisha. Ufalme unaoanzishwa ni wa hapa katika dunia. Mungu anaongoza kutoka katika mbingu, lakini mpango wake ni kumtuma Yesu kuitawala dunia. Wafuasi wake walio waaminifu wa enzi zote watakuwa watu wa kumsaidia katika jukumu hili kubwa.

Yesu alidai kuwa ni Mfalme. Kwenye kesi yake wakati Pilato alipomuuliza, “Wewe u Mfalme basi?”, yeye alijibu, akisema: “Wewe wasema, kwa kuwa mimi ni mfalme” (Yohana 18:37). Hii ni namna ya Kiyahudi ya kusema, “Ndiyo!”

Juu ya msalaba Yesu aliosulubiwa, iliandikwa, “HUYU NI YESU, MFALME WA WAYAHUDI” (Mathayo 27:37).  Maadui zake walidhani wanamdhihaki; hawakujua kuwa wanachosema ni KWELI.

Injili aliyoihubiri Yesu ilikuwa ni Habari Njema ya huo Ufalme wa Mungu. Katika Luka 8:1, tunasoma kuwa: “Alikuwa akizunguka-zunguka katika miji na vijiji, akihubiri na kuitangaza habari njema ya Ufalme wa Mungu”.

Sasa unajua sababu ya kurudi kwake Yesu. Anarudi kuusimamisha tena Ufalme wa Mungu katika dunia.

KITI CHA ENZI CHA DAUDI KATIKA YERUSALEMU

UFALME WA ISRAELI

Wafalme katika Kiti cha Enzi

Daudi, Sulemani…………

VITABU:Samweli na Wafalme; kama 1000 K.K.

KITI CHA ENZI KITUPU

Hakuna Wafalme…..

 

KITABU: EZEKIELI 21:27

600 K.K. Leo(tulipo)

YESU: Kurudi kutoka mbinguni; kuusimamisha Ufalme wa Mungu duniani. KITABU: LUKA 1:32

Mbeleni ………….

Ufalme huo na sisi

Pengine unaweza kufikiri, kwa nini, basi, tuombe ‘Ufalme wako uje’, wakati Ufalme wenyewe ni wa Kiisraeli?  Unatuhusu nini sisi?

Unavyoendelea kujifunza utagundua kuwa, Ufalme huo ambao Yesu atauongoza, utapanuka sana na kuenea maeneo ya mbali, kuliko ilivyokuwa kwa ule Ufalme wa Mungu wa kwanza. Utaenea dunia yote, na kuleta amani kwa watu wote.

Kwa hiyo tunauombea Ufalme wake uje, na tunaomba pia kwamba, Yesu atakaporudi aweze kutuambia: “Njoni mliobarikiwa na Baba yangu, urithini Ufalme mliowekewa tayari tangu kuumbwa ulimwengu” (Mathayo 25:34).

Muhtasari- Ona vile kila sehemu ya Biblia inavyosaidia kuelezea sehemu nyingine. Sasa tumejifunza kuwa:

  1. Ufalme wa Mungu uliwahi kuwepo katika nchi ya Israeli.
  2. Mungu aliusitisha Ufalme huo, lakini aliahidi huurudishia upya na kumpa anayeustahili.
  3. Mrithi huyo ni Yesu, na atakikalia hicho Kiti cha Enzi cha Daudi katika Yerusalemu, akiwatawala Wayahudi na ulimwengu wote.
  4. Waaminifu wote wataishiriki mibaraka ya Ufalme huo katika dunia.

Vifungu vya kusoma:  Mwanzo 22,  Wagalatia 3

Jifunze kwa moyo: Ufunuo 11:15

“Malaika wa saba akapiga baragumu, pakawa na sauti kuu katika mbingu, zikisema, Ufalme wa dunia umekwisha kuwa ufalme wa Bwana wetu na wa Kristo  wake, naye atamiliki hata milele na milele”.

Swahili Title
Ufalme wako uje - Somo la 09
Swahili file
PDF file
African text
Christadelphian Bible Mission