Ahadi za Mungu kwa Daudi - Somo la 15

Swahili

Somo la 15

AHADI ZA MUNGU KWA DAUDI

Somo: 2 Samweli 7

Kijana mchunga-kondoo awa mfalme

Utakuwa pengine umesikia juu ya Daudi, kijana aliyekuwa mchungaji wa kondoo, aliyemuua Goliati, mtu wa ‘maraba mitatu’ kwa kijiwe kimoja alichomtupia.

Daudi aliishi kama miaka 1000 kabla ya Yesu Kristo kuzaliwa. Alizaliwa katika eneo moja na Yesu, katika mji mdogo karibu na Yerusalemu uitwao Bethlehemu. Alikuwa mwana wa kiume wa mwisho wa Yese, aliyekuwa mmiliki wa hao kondoo.

Wakati Daudi alipokuwa bado mdogo Mungu alimtuma nabii wake, Samweli, ampake mafuta ya kuwa mfalme juu ya Israeli. Lakini kwa wakati huo, mfalme Sauli, aliyekuwa mfalme wa kwanza wa Israeli, alikuwa akitawala. Sauli alimuonea sana wivu Daudi, na kwa nyakatii mbalimbali alijaribu kumuua. Matokeo yake yalikuwa Daudi kumkimbia na kuwa mkimbizi.

Sauli hakuwa mfalme mzuri; hakumtii Mungu. Wakati ulifika akauawa katika pambano na Wafilisti. Hapo ndipo njia ilipofunguka kwa Daudi kuwa mfalme.

Baada ya majaribu mengi na harakati, Daudi alijenga Ikulu yake katika Yerusalemu, na ndipo alipoishi na kutawala.

Daudi alipofikiria jinsi Mungu alivyombariki na juu ya sanduku lake ambalo bado lilikuwa likikaa katika hema, alitaka kujenga Hekalu zuri katika Yerusalemu ambalo sanduku hilo lingehifadhiwa ndani yake. Sanduku hilo lilikuwa sanduku ambamo ndani yake kuliwekwa kibao cha Amri-kumi za Mungu, na lilikuwa na kifuniko kilipowekwa juu yake ‘kiti cha rehema’. Juu yake utukufu wa Mungu uling’aa.

Daudi alimwambia alichotaka kufanya Nathani, nabii wa Mungu. Nathani alimjibu Daudi kwa kumwambia aendelee, lakini usiku huo Mungu alisema na Nathani, na kumpa ujumbe maalum sana kwa Daudi.

Ujumbe wa Mungu kwa Daudi

Fungua tena 2 Samweli, Sura ya 7. Sehemu ya muhimu sana ya ujumbe huo wa Mungu kwa Daudi, upo katika mstari wa 12 mpaka wa 16. Hapa Mungu anamuahidi Daudi kupata mtoto wa kiume. Anasema juu ya ‘mzao’ huyo kuwa:

“Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu, nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele” (ms. 13).

Hili lilikuwa litokee baada ya Daudi kufa, kwa kuwa anaambiwa katika mstari wa 12 kuwa, ni hapo, “Siku zako zitakapotimia, ukalala na baba zako”.

Zaidi juu ya huyo Mwana wa Daudi

Sasa Daudi alipata mwana aliyemwita Sulemani, aliyetawala baada yake katika Yerusalemu. Ahadi alizokuwa amepewa Daudi, kwa sehemu zilitimia katika Sulemani, lakini utimilifu wa ahadi hizo ulibidi usubiri ujio wa Bwana Yesu. Sulemani alifanywa mfalme wakati Daudi akiwa bado hai, na kwa vyovyote Sulemani hakutawala milele; alikufa.

Huyo mwana Daudi aliyekuwa ameahidiwa hasa, alikuwa awe mtu wa kipekee sana, kwa kuwa Mungu anasema juu yake kuwa:

“Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu” (2 Samweli 7:14).

Tugeukie Sura ya kwanza ya Luka. Hapa tunasoma juu ya malaika wa BWANA, aliyemtokea msichana mmoja, mmojawapo wa watu wa ukoo wa mfalme Daudi na kumwambia, atazaa mtoto wa kiume. Huyo alikuwa azaliwe, sio kwa njia ya kawaida ya baba wa kidunia, kama inavyokuwa kwa watoto wote. Alikuwa azaliwe kwa muujiza wa uweza wa Mungu. Mwanamke huyu aliyekuwa bado bikira, aliyeitwa Mariamu, aliambiwa:

“Roho Mtakatifu atakujilia juu yako, na nguvu zake Aliye-juu zitakufunika kama kivuli, kwa sababu hiyo hicho kitakachozaliwa kitaitwa kitakatifu, Mwana wa Mungu” (Luka 1:35).

Malaika alimwambia tena Mariamu:

“Huyo atakuwa mkuu, ataitwa Mwana wa Aliye juu, na Bwana Mungu atampa kiti cha enzi cha Daudi, baba yake. Atamiliki nyumba ya Yakobo hata milele, na ufalme wake utakuwa hauna mwisho” (Luka 1:32,33).

Sasa tunaweza kuona jinsi ahadi Mungu aliyompa Daudi, ilivyotimia alipozaliwa Yesu Kristo:

  1. Mungu alikuwa ndiye Baba yake.
  2. Yesu amewekewa atawale milele.

Mfalme wa Wayahudi

Yesu alizaliwa awe Mfalme. Mamajusi walipokuja kumsujudia Yesu, waliuliza, “Yuko wapi yeye aliyezaliwa mfalme wa Wayahudi?” (Mathayo 2:2).

Yesu alipokamatwa na kupelekwa kwa Pilato ahukumiwe, Pilato alimuuliza: “Wewe ndiwe mfalme wa Wayahudi?” Yesu alimjibu kwa kusema, “Wewe wasema” (Marko 15:2). Hii ni namna ya Kiyahudi ya kusema: “Ndiyo, kwa hakika ndiye”. Kama ambavyo tumekwisha kuona, Yesu atarudi katika dunia hii na kuwa Mfalme wa Wayahudi; na kutawala katika kiti cha enzi cha Daudi.

Ufalme wa dunia yote

Yesu hatakuwa Mfalme wa Wayahudi tu atakaporudi. Atakuwa Mfalme wa dunia nzima. Mungu alisema hivi juu yake: “Ni neno dogo sana wewe kuwa mtumishi wangu, ili kuziinua kabila za Yakobo, na kuwarejesha watu wa Israeli waliohifadhiwa; zaidi ya hayo nitakutoa uwe nuru ya mataifa, upate kuwa wokovu wangu hata miisho ya dunia” (Isaya 49:6). ‘Mataifa’ maana yake ni, ‘Watu wasio Wayahudi’.

Daudi Je?

Ingawa Daudi alitambua kuwa ahadi hiyo ya Mungu isingetimizwa kwa kipindi kirefu sana, alikuwa na shukrani sana kwa Mungu. Tunaweza kusoma maombi yake ya kushukuru katika 2 Samweli 7:18-29. Mungu alimwambia:

“Na nyumba yako, na ufalme wako, vitathibitishwa milele mbele yako” (2 Samweli 7:16). Maana yake ni akiwepo.

  • ‘Nyumba’ inaweza kuwa na maana ya jengo. Hekalu liliitwa, ‘Nyumba ya Mungu’. Lakini ‘nyumba’ inaweza kuwa na maana pia ya familia au ukoo, na hiki ndicho kinachomaanishwa katika ahadi hizi kwa Daudi.

Kwa hiyo Daudi mara nyingi aliifikiria hiyo ahadi, au agano, ambalo Mungu alikuwa amempa na analiongelea katika Zaburi. Kwa mfano, katika Zaburi 89: 2-4 analikumbuka likisema:

“Maana nimesema, Fadhili zitajengwa milele, katika mbingu utauthibitisha uaminifu wako. Nimefanya agano na mteule wangu, nimemuapia Daudi, mtumishi wangu. Wazao wako nitawafanya imara milele, nitakijenga kiti chako cha enzi hata milele”.

AHADI ZA MUNGU KWA DAUDI (2 Samweli 7)

Andiko

Ms. 12: “Siku zako zitakapotimia ukalala na baba zako, nitainua mzao wako nyuma yako, atakayetoka viunoni mwako, nami nitafanya imara ufalme wake”.

Muhtasari

Maisha ya Daudi yalipokwisha, alikufa.

Mungu angemwinua mmoja kati ya wazaliwa wake, na Mungu angeusimamisha tena Ufalme wake.

Ms. 13: “Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa jina langu,

Huyo ‘mzao’ atamjengea Mungu nyumba. Sulemani alimjengea Mungu nyumba. Yesu Kristo anamjengea Mungu nyumba hata sasa (Soma Waefeso 2:19-22).

…nacho kiti cha enzi cha ufalme wake nitakifanya imara milele”.

Mungu atafanya ufalme wake imara milele. Sulemani hakutawala milele, wala Ufalme wa Israeli haukudumu milele. Yesu ndiye atakayetawala milele.

Ms. 14: “Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwanangu;

akitenda maovu, nitamwadhibu…”

Mungu atakuwa ndiye baba kwa mzaliwa huyu wa Daudi, naye atakuwa Mwana wa Mungu. Yesu ni mwana wa Mungu.

Yesu hakutenda dhambi, hivyo Mungu hakulazimika kumwadhibu.

Ms. 16: “Na nyumba yako, na ufalme wake, vitathibitishwa milele mbele yako.

Nacho kiti chako kitafanywa imara milele”.

Nyumba ya Daudi na ufalme vitasimamishwa, na Daudi atakuwa yupo hapo. Hili litatokea hapo Yesu atakaporudi. Daudi atafufuliwa  kutoka kwa wafu na kuwa katika Ufalme huo.

Yesu kwa wakati huo atakuwa akitawala kutoka katika kiti cha enzi cha Daudi (Yerusalemu). Ufalme wake utakuwa hauna mwisho.

Kitu cha kutazamiwa

Paulo anatuambia kwenye Waebrania 11:39,40 kuwa:

“Na watu hao wote wakiisha kushuhudiwa kwa sababu ya imani yao, hawakuipokea ahadi, kwa kuwa Mungu alikuwa ametangulia kutuwekea sisi kitu kilicho bora, ili wao wasikamilishwe pasipo sisi”.

Sasa, Ibrahimu na Daudi na waaminifu wengine wengi, walikufa wakijua kuwa, katika siku ya kuja kwa Yesu Kristo, watafufuliwa tena na ‘kukamilishwa’. Watapewa uzima wa milele na wote wale walio wa Kristo. Lakini kama kifungu hicho kinavyoonesha, uzima wa milele hautakuwa kwa ajili ya watu hao waaminifu tu, unaweza ukawa wetu pia.

Msitari wa msingi

Tumeona kwamba Yesu Kristo ni mzao wa Ibrahimu, na mzao wa Daudi. Msitari wa kwanza kabisa wa Agano Jipya, unaanza na:

“Kitabu cha ukoo wa Yesu Kristo, mwana wa Daudi, mwana wa Ibrahimu” (Mathayo 1:1).

Kwa hiyo tunaweza tu kulielewa Agano Jipya, kama tumelisoma na kulielewa Agano la Kale.

Muhtasari

  1. Mungu alimuahidia Daudi mwana.
  2. Mwana huyo alikuwa ni Yesu, Mwana wa Mungu.
  3. Amewekewa kuwa Mfalme; atawale katika Kiti cha Enzi cha Daudi milele.
  4. Atakaporudi kutawala, watumishi waaminifu wote wa Mungu watapewa uzima usio na mwisho, na watashirikishwa katika Ufalme wake huo katika dunia.

Vifungu vya Kusoma:  2 Samweli  7, 1 Nyakati 17.

Jifunze kwa moyo:      1 Nyakati 17 : 11,  12

“Na itakuwa, siku zako zitakapotimia, uende na babazo, nitainua mzao wako nyuma yako, atakayekuwa wa wana wako, nami nitakifanya imara kiti cha enzi cha ufalme wake milele”.

Swahili Title
Ahadi za Mungu kwa Daudi
Swahili file
PDF file
Arabic file
African text
Christadelphian Bible Mission