Baba na Mwana - Somo la 16

Swahili

Somo la 16

BABA NA MWANA.

SOMO: Isaya 45

“Je! Wewe waweza kuuvumbua ukuu wa Mungu?” (Ayubu 11:7)

Hili swali liliulizwa maelfu ya miaka iliyopita. Jibu lake ni lile lile leo kama lilivyokuwa kwa siku hizo; kwa vyovyote hatuwezi! Hakuna kitu kabisa tunachoweza kujua kumhusu Muumbaji Mkuu wa vitu vyote, nje ya yale Yeye Mwenyewe anayotuambia katika Neno lake; katika Biblia. Hata hivyo hakuna tumaini la uzima wa milele tunaloweza kulipata, bila ya huko kumjua.

Njia pekee ya kuweza kumjua Mungu ni kwa kukisoma kitabu chake, Biblia, au kulisikiliza Neno lake, alilotupa. Mungu mwenyewe amesema:

“Mawazo yangu si mawazo yetu, wala njia zenu si njia zangu, asema BWANA. Kwa maana kama vile mbingu zilivyo juu sana kuliko nchi, kadhalika njia zangu zi juu sana kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu” (Isaya 55:8,9).

Mungu ni Mmoja

“Sikiliza, Ee Israeli, BWANA, Mungu wetu, BWANA ndiye mmoja. Nawe mpende BWANA, Mungu wako, kwa moyo wako wote, na kwa roho yako yote, na kwa nguvu zako zote” (Kumb. La Torati 6:4,5).

Musa aliyasema maneno haya kwa Waisraeli wakiwa nyikani. Ujumbe kwamba ‘Mungu ni mmoja’, umerudiwa-rudiwa mara nyingi katika Maandiko. Katika Isaya 45:5 tunaambiwa:

“Mimi ni BWANA, wala hapana mwingine, zaidi yangu mimi hapana Mungu”.

Miaka zaidi ya elfu baada ya hapo, mtume Paulo anasema kitu hicho hicho.

“Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, mwanadamu Kristo Yesu” (1 Timotheo 2:5). Na tena, katika 1 Timotheo 6:15,16 Paulo anamuongelea Mungu kuwa ni:

“Yeye aliyehimidiwa, Mwenye uweza peke yake, Mfalme wa wafalme, Bwana wa mabwana; ambaye yeye peke yake hapatikani na mauti, amekaa katika nuru isiyoweza kukaribiwa; wala hakuna mwanadamu awezaye kumwona. Heshima na uweza una yeye hata milele. Amina”.

Huyu Mungu aliye mtakatifu ni Mungu wa upendo.

Kama Biblia ingetuambia tu juu ya uweza na utakatifu wa Mungu, kwa vyovyote tungemcha, lakini tungeona shida kumpenda. Lakini Mungu ametuonesha kuwa, yeye pia ni mwema na amejaa huruma. Mwandika Zaburi anatuambia kuwa:

“BWANA amejaa huruma na neema, haoni hasira upesi, ni mwingi wa fadhili…. Kama vile baba wahurumiavyo watoto wake, ndivyo BWANA anavyowahurumia wamchao. Kwa maana, Yeye anatujua umbo letu, na kukumbuka ya kuwa sisi tu mavumbi” (Zaburi 103: 8,13,14).

Ni katika huruma na upendo wake, Mungu ametupa Bwana Yesu Kristo kuzichukua dhambi zetu.

Mwana wa Mungu

Tangu mwanzo Mungu alikuwa amepanga kumtuma Mwanawe kutuokoa. Kuna utabiri mwingi kumhusu Yesu katika Agano la Kale. Katika Isaya 7:14, kwa mfano, tunaambiwa:

“Tazama, bikira atachukua mimba, atazaa mtoto mwanamume, naye utamwita jina lake Imanueli”.

Maana ya Imanueli ni ‘Mungu pamoja nasi’. Mungu hapa anaahidi kumtuma Mwanawe mwenyewe. Angalia vifungu vingine hivi vinavyoonesha kuwa Yesu ni Mwana wa Mungu:

Wagalatia 4:4

“Hata ulipowadia utimilifu wa wakati, Mungu alimtuma Mwanawe ambaye amezaliwa na mwanamke, amezaliwa chini ya sheria.

 

Marko 1:11

“Na sauti ikatoka mbinguni, Wewe ndiwe Mwanangu, mpendwa  wangu, nimependezwa nawe” (Mungu alisema hili katika ubatizo wa Yesu).

 

Yohana 20:31

“…….ili mpate kuamini ya kwamba, Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu; na kwa kuamini mwe na uzima kwa jina lake.

Yesu hakuwapo kabla

Mtoto anapozaliwa, ndipo maisha mapya yanapoanza. Kuzaliwa kwa Yesu Kristo hakukuwa na utofauti.

Kuna watu wanaofikiri kuwa, Bwana Yesu Kristo alikuwepo kabla hajazaliwa na Mariamu. Kwa sehemu mtu anaweza kusema hivyo, kama ni kwa kumaanisha kuwa Mungu alishapanga tokea mwanzo kuwa angepata Mwana.

Mungu anapopanga kitu, tunajua kwa uhakika kabisa kuwa kitatokea. Yesu Kristo ni msingi wa kusudi la Mungu; ni mhimili wa mpango wote mkubwa wa wokovu. Kwa hiyo, Mungu alipokuwa akiwaambia waaminifu wa kale katika Agano la Kale kuhusiana na mpango wake huo, aliwaambia juu ya Kristo.

Kwa namna hiyo hiyo Biblia inamwongelea Kristo kuwa ni: “Mwana-kondoo aliyechinjwa tangu kuwekwa misingi ya dunia” (Ufunuo 13:8). Hili halina maana kuwa Yesu alichinjwa kabla dunia haijaumbwa au wakati ikiumbwa. Tukio hili la kutisha lilitokea mara moja tu kama miaka 2000 iliyopita, Yesu aliposulubiwa (Waebrania  9:25–28).

Kwa kuwa kifo cha Yesu ni cha msingi sana katika kusudi la Mungu, Mwenyezi Mungu amekiongelea kama tukio lililo la muhimu sana linalowagusa watu wa nyakati zote, tangu wakati wa Agano la Kale. Kwa hiyo, ni kifo cha Yesu ambacho kimeyabadili mambo yote, “tangu kuwekwa misingi ya dunia”.

Biblia inatumia lugha ya kuwepo-kabla katika kumwelezea Bwana Yesu, lakini haina maana kuwa tayari alishakuwepo; akiishi kabla ya kuzaliwa kwake. Alikuwepo, ndiyo, lakini ni katika mawazo ya Mungu. Mungu alipanga kufanya Yesu azaliwe kwa wakati aliouweka, ‘katika utimilifu wa nyakati’ (Waebr. 9:26).

Ni pale Mariamu alipomzaa mtoto wake huyo wa kiume wa kwanza, ndipo Bwana Yesu alipoanza kuwepo; alipoanza kuishi. Ni kama inavyokuwa kwetu.

Asili ya Yesu

Kwa kuwa Yesu alizaliwa na mwanamke, alikuwa na hulka kama ya kwetu. Katika Waebrania 2:17 tunaambiwa:

“Kwa hiyo ilimpasa kufananishwa na ndugu zake katika mambo yote”.

Wakati wa uhai wake hapa duniani, alijaribiwa kwa namna nyingi, lakini hakuwahi kuanguka dhambini. Hebu vitazame vifungu hivi, vyote vikiwa vimechukuliwa kutoka katika kitabu kwa Waebrania, kuona kuwa Yesu alikuwa na hulka kama yetu, alipokuwa akiishi hapa duniani:

Waebrania 4:15

“Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu, bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi”.

Waebrania 2:14

“Basi, kwa kuwa watoto wameshiriki damu na mwili, yeye naye vivyo hivyo alishiriki yayo hayo, ili kwa njia ya mauti amharibu yeye aliyekuwa na nguvu ya mauti, yaani, Ibilisi”.

Waebrania 2:9

“Ila twamwona yeye aliyefanywa mdogo punde kuliko malaika, yaani, Yesu, kwa sababu ya maumivu ya mauti, amevikwa taji ya utukufu na heshima, ili kwa neema ya Mungu aionje mauti kwa ajili ya kila mtu”.

Waebrania 5:7,8

“Yeye, siku hizo ya mwili wake, alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu, na, ingawa ni Mwana, alijifunza kutii kwa mateso hayo yaliyompata”.

Kwa vyovyote, Yesu alikuwa hivi kabla ya kufa na kufufuka kwake tu. Baada ya kufufuka alipewa hulka tofauti ya utukufu na nguvu; hulka ya kutoweza kufa tena.

Wazo potofu

Watu wengi wameyapuuzia mafundisho ya Biblia yanayomhusu Mungu, na kuja kuamini kitu wanachokiita, “Utatu Mtakatifu”. Wanasema kuwa Mungu anazo nafsi tatu: Baba, Mwana na Roho Mtakatifu, na wote wako sawa. Hakuna ukweli juu ya dhana hii. Tutatafakari kuhusu Roho Mtakatifu mbeleni kidogo, kwenye Somo la 20.

Maneno ‘Utatu-Mtakatifu’ na ‘Mungu-Mwana’ hayapo kabisa katika Biblia. Tumekwishaona mafundisho ya moja kwa moja ya Biblia kuwa Mungu ni mmoja, na kwamba Yesu ni Mwanawe. Kama vile mwana aliye mwema anavyokuwa chini ya baba yake, ndivyo Yesu alivyokuwa chini ya Mungu.

Yesu hakuwahi kudai kuwa yuko sawa na Mungu, bali alimtegemea Baba yake kwa mambo yote. Alisema, “Mwana hawezi kutenda neno mwenyewe ila lile ambalo amwona Baba analitenda” (Yohana 5:19).

Ni kweli kwamba Yesu aliwahi kusema: “Mimi na Baba tu umoja” (Yohana 10:30). Alikuwa na maana kuwa, yeye na Baba yake walikuwa wamoja kidhamira na kimalengo, na aliomba umoja huo uwepo pia kati Yao na wafuasi (Yohana 17:21). Tunaambiwa:

“Basi, vitu vyote vikiisha kutiishwa chini yake(Yesu), ndipo Mwana mwenyewe naye atatiishwa chini yake yeye aliyemtiishia vitu vyote, ili kwamba Mungu awe yote katika wote” (1 Wakorintho 15:28).

Mstari huu unatuambia kuwa, hata baada ya utawala wa Yesu wa miaka 1000 katika dunia, ambao ni kipindi cha Ufalme wa Mungu katika dunia, Yesu ataendelea kuwa chini ya Baba yake, na Mungu atakuwa yote katika wote.

Imani ya ‘Utatu’ ilitoka wapi?

Wakristo wa awali hawakuamini ‘Utatu’. Waliamini kile Biblia inachofundisha, kuwa: “Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja, mwanadamu Kristo Yesu” (1 Tim 2:5).

Sasa, mambo haya potofu ya ‘utatu’ yalitoka wapi?

Ilikuwa imepita miaka zaidi ya 300 baada ya kuzaliwa kwa Yesu, ‘Wakristo’ walipoanza kuamini katika ‘utatu’. Wazo hilo halikuwa na msingi katika Biblia, badala yake lilitokana na imani za kale za Wayunani, ambao hawakuwa wakijua lolote kumhusu Mungu mmoja pekee Aliye wa Kweli. Pole pole, kanisa lililichukua wazo hilo la ‘Mungu mmoja katika nafsi tatu’, na kuukana ukweli wa Biblia unaomhusu Mungu.

‘Imani ya Mitume’ iliyotungwa kama miaka 100 baada ya Kristo kupaa kwenda mbinguni, inaonesha imani waliyokuwa nayo Wakristo wa awali, Wakristo wa kwanza. Inasomeka hivi:

“Namwamini Mungu Baba, Mwenye uweza wote, Muumba wa mbingu na nchi. Namwamini Yesu Kristo, Mwana wake wa pekee, Bwana wetu. Aliyechukuliwa mimba kwa uwezo wa Roho Mtakatifu, akazaliwa na mwanamwali Mariamu………”

Hiki ndicho hasa Biblia inachofundisha (tofauti na imani zingine). Ukuu na uweza wa Mungu ni vitu ambavyo viko nje ya uwezo wetu wa kufikiri. Tunajikuta tukishindwa kuelewa hasa-hasa jinsi Mungu huyu wa milele alivyoweza kupata mtoto na msichana huyu wa kimwili na damu, lakini yeye Mungu anatuambia ndivyo ilivyokuwa. Tunajua Neno lake ni kweli; wajibu wetu ni kulipokea hivyo kwa imani.

Kama tunahitaji kumpendeza Mungu, ni lazima tulipokee lile analotuambia bila kuongezea mawazo ya kibinadamu yasiyo kwenye Biblia.

Muhtasari

  1. Kuna Mungu mmoja tu.
  2. Mungu sio ‘watatu katika mmoja’.  Mafundisho ya Utatu Mtakatifu hayapo kwenye Biblia.
  3. Yesu Kristo ni Mwana wa Mungu, aliyezaliwa na mwanamwali Mariamu. Yesu Kristo sio Mungu-mwana.
  4. Yesu alikuwa ni mwanadamu, lakini kwa kuwa Mungu alikuwa ni Baba yake, alikuwa na utofauti wa muhimu na mwanadamu mwingine yeyote. Kwa kushinda dhambi amekuwa Mkuu juu ya wote.
  5. Kuzaliwa kwa Yesu kulikuwa ni muujiza, kwa kuwa mama yake alikuwa bikira. Baba yake alikuwa ni Mwenyezi Mungu.

  Vifungu vingine vya kupitia.

Yesu alianza kuishi alipozaliwa.

1 Petro 1:20, Waebrania 9:26

Yesu alikuwa ni mtu.

Matendo 2:22, Wafilipi 2:8, Waebrania 2: 9, 14 – 18.

Mungu ni Mkuu kuliko Yesu

Waefeso 4: 6, 1 Wakorintho 11:3, Yohana 14: 28, Yohana 10: 29.

Vifungu vya kusoma:     Kumb. la Torati 6, Mathayo 1:18–25.

Jifunze kwa moyo:        1 Timotheo 2:5

“Mungu ni mmoja, na mpatanishi kati ya Mungu na wanadamu ni mmoja; mwanadamu Kristo Yesu”.

 

Swahili Title
Baba na Mwana
Swahili file
PDF file
Arabic file
African text
Christadelphian Bible Mission